Friday 22 May 2015

WAWAKILISHI ZANZIBAR WAIBANA TUME YA UCHAGUZI (ZEC)

WAJUMBE WA Baraza la Wawakilishi wameitaka Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kusimamia Uchaguzi Mkuu kwa kufuata misingi ya sheria na katiba ili kuepuka vurugu.


Wakichangia makadirio mapato na matumizi ya bajeti ya Wizara ya Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mwakilishi wa Jimbo la Wete, Asaa Othman alisema vurugu za kisiasa Zanzibar hujitokeza kipindi cha Uchaguzi Mkuu na mara Tume inapotangaza matokeo ya urais.

Alisema matarajio ya wananchi wengi, kuona ZEC iliyopewa jukumu la kusimamia uchaguzi inatekeleza majukumu yake kwa kufuata matakwa ya kikatiba na sheria na sio kuhubiri ushabiki wa kisiasa.

“Mwaka huu tunakabiliwa na matukio mawili makubwa Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa pamoja na Uchaguzi Mkuu ambapo matarajio yetu makubwa kuona utulivu wa kisiasa unadumishwa katika kipindi chote hicho na kuepuka 
matukio ya fujo,” alisema Mhe Asaa.

Mwakilishi wa Jimbo la Micheweni, Subeit Khamis Faki (CUF) aliitaka ZEC kusimamia uchaguzi kama ilivyofanya katika mwaka 2010, ambapo matukio ya fujo na vurugu za kisiasa zilidhibitiwa.

Aidha aliitaka Tume ya Uchaguzi kusimamia vizuri kazi za uandikishaji na uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura ambalo litawawezesha wananchi kutumia haki ya kidemokrasia kupiga kura.

Aliitaka tume kufanya kazi ya kuwaandikisha wapiga kura wenye sifa ya kushiriki katika uchaguzi mkuu, na wale ambao hawastahiki wasiorodheshwe.

“Kazi ya uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura imeanza katika kisiwa cha Pemba, lakini tunaiomba ZEC kuhakikisha kwamba watu wenye sifa tu ndiyo wanaoandikishwa katika daftari hilo,” alisema Mhe Subeit.

Mwakilishi wa Viti Maalumu, Mwanaidi Kassim Mussa (CCM) aliipongeza Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar kwa kufanya kazi za kusimamia daftari la kudumu la wapiga kura vizuri.

Alizitaja miongoni mwa kazi ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ni kuboresha daftari la kudumu la wapigakura ambalo litatoa nafasi kwa wananchi kushiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

“Tunaipongeza Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar kwa kufanya kazi zake vizuri ambazo zimeiwezesha kusimamia uchaguzi mkuu vizuri kwa mafanikio mwaka 2010,” alisema Mhe Mwanaidi.

Mwakilishi wa Jimbo la Amani, Fatma Mbarouk Said (CCM) aliitaka Serikali kudhibiti amani na utulivu kuelekea katika uchaguzi mkuu kwa ajili ya kuhakikisha makundi ya wanawake na watoto yanakuwa salama.

Alisema uzoefu unaonesha kwamba katika fujo za uchaguzi mkuu waathirika wakubwa ni wanawake na watoto kutokana na mazingira yao kwa ujumla:

“Tunaiomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kudhibiti amani na utulivu kuelekea uchaguzi mkuu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba jamii yetu inakuwa salama ikiwemo wanawake na watoto,’’ alisema Mhe Fatma.

Mwakilishi wa Viti Maalumu, Panya Ali Abdallah (CCM) amewataka baadhi ya wanasiasa kuacha kuingilia majukumu ya Tume ya Uchaguzi.

Alisema katika siku za hivi karibuni wapo viongozi wa kisiasa ambao wamekuwa wakitoa kauli za kushutumu majukumu ya tume iliyopewa kwa mujibu wa katiba na sharia:

“Mheshimiwa Spika nawaomba viongozi wa vyama vya siasa kuacha kutoa kauli za shutuma kwa taasisi iliyopewa majukumu ya kusimamia uchaguzi mkuu (ZEC) kwani kufanya hivyo ni sawa kuinyima uhuru wa majukumu yake,’’ alisema Mhe Panya.