Sunday 10 May 2015

JOHN NYERERE KUAGWA LEO


MAMIA ya wakazi wa Dar es Salaam leo wanatarajia kutoa heshima za mwisho kwa John Nyerere (58), ambaye ni mmoja wa watoto wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

John alifariki dunia juzi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, alikokuwa amelazwa.

Makongoro Nyerere ambaye ni mtoto mwingine wa Mwalimu Nyerere, alisema Dar es Salaam jana kuwa mwili wa John utasafirishwa kesho kwenda Mwanza na kisha kupelekwa kijijini kwao Butiama Mkoa wa Mara kwa maziko.

“Misa ya kumuombea John itafanyika hapa Msasani nyumbani kwa Mwalimu na kufuatiwa na utoaji wa heshima za mwisho,” alisema Makongoro, ambaye ni Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki.

John alitumikia Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na alishiriki Vita vya Kagera vya 1978 na 1979, vilivyolenga kumng’oa nduli Iddi Amin wa Uganda.
Watoto wengine wa Mwalimu ni Andrew, Magige, Madaraka, Anna na Rose.