Monday 16 March 2015

SERIKALI YA ZANZIBAR HAIFANYI BIASHARA KATIKA SEKATA YA AFYA BALI HUWATAKA WANANCHI KUCHANGIA HUDUMA HIZO




Na Kijakazi Abdalla- Maelezo Zanzibar

Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Mahmoud Thabiti Kombo amesema hospitali za Zanzibar hazifanyi biashara ya vipimo vya aina yoyote katika maabara zake bali huwataka wananchi kuchangia kwa baadhi ya vipimo hivyo na kupewa risiti mara baada ya kuchangia huduma hiyo.


Hayo ameyaeleza wakati akijibu swali la mwakilishi wa Jimbo la Muyuni Mhe. Jaku Hashim Ayoub katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi huko Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja.

Amesema kuwa ipo haja kwa wananchi kudai risiti ya malipo wakati wanapochangia huduma hiyo ili iwe ndio uthibitisho wa malipo hayo na endapo ikitokea kwa mwananchi yoyote kutopewa risti hiyo kwa ajili ya huduma aliyochangia anatakiwa kutoa taarifa kwa uongozi wa hospitali aliyolipia au kutoa taarifa kwa watendaji wa wizara hiyo.

Aidha amesema kuwa uongozi wa Wizara hiyo hauna taarifa juu ya kuwepo kwa wizi wa baadhi ya vifaa vya matibabu na kuuzwa kwa wananchi kutoka kwa watendaji wa wizara hiyo hivyo amesema Wizara yake italifanyia kazi tatizo hilo ipasavyo ili kulipatia ufumbuzi unaofaa na kuwataka wananchi kushirikiana na Serikali kwa kutoa taarifa pindi wanapobaini kuwepo kwa tatizo hilo kwa maslahi yao na Taifa kwa ujumla.

Wakati huohuo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema kuwa kupitia Wizara yake ya Biashara, Viwanda na Masoko inafanya juhudi za makusudi kwa lengo la kuwasaidia Wajasiriamali kuweza kuuza bidhaaa zao katika masoko ya ndani na nje Nchi.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar Mhe. Thuwaiba Edington Kisasi katika kikao cha Baraza la Wawakilishi huko Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja, wakati akijibu swali la mwakilishi wa nafasi za wanawake Mhe. Shadya Mohammed Suleiman.

Mhe. Kisasi amesema Wizara yake imekuwa ikichukuwa juhudi mbalimbali katika kuzitafutia masoko ya nje bidhaa zinazozalishwa Zanzibar, juhudi hizo ni pamoja na kutumia soko la Jumapili ambalo lilianzishwa rasmi huko Pemba kwa Wajasiriamali wanaouza bidhaa zao ndani ya Kisiwa cha Pemba.

Aidha amesema kuwa Soko hilo lina jumla ya vikundi 28 hadi sasa ambavyo vinashiriki kikamilifu katika maonyesho mbalimbali ya biashara pamoja na kuandaa na kuratibu ushiriki Wajasiriamali wa Zanzibar katika maonesho hayo na Matamasha ya Biashara ya ndani na nje ya Zanzibar.

Hata hivyo Naibu Waziri huyo amesema kuwa katika maonesho ya Sabasaba yaliyofanyika Mwaka jana jumla ya wajasirmali 48 kutoka Zanzibar walishiriki maonyesho hayo ambapo wajasiriamali 19 kutoka Pemba na 29 kutoka Unguja, pamoja na hayo juhudi hizo zimeshaanza kuzaa matunda na wajasiriamali wameanza kupata masoko zaidi kwa kwa ajili kuuza bidhaa zao.