Saturday 14 March 2015

Serikali itaendelea kuharakisha na kuimarisha miundombinu ya barabara


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Wananchi wa Mtambwe baada kutembelea bara bara za ndani zinazojengwa kwa msaada wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo ( IFAD ).


Balozi Seif akawataka kushirikiana na wawekezaji walioamuwa kuweka miradi yao ya kiuchumi katika maeneo yao ili nao wapate ajira na kuongeza kipatyo chao cha kila siku.



Afisa Mdhamini Wizara ya Miundo Mbinu na Mawasiliano Pemba Nd. Hamad Ahmed Baucha akimpatia maelezo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif kuhusu ujenzi wa Bara bara ya Ole- Kengeja inayogharamiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Kulia ya Balozi Seif ni Mhandisi Muelekezi wa ujenzi wa Bara abara hiyo Ndugu Remidius Edington Kisasi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alisema kwamba dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuharakisha miundo mbinu ya Mawasiliano ya Bara bara  ili kuwapa fursa nzuri Wananchi wake kupata huduma zilizo bora  za usafiri.

Balozi Seif alisema hayo wakati akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Mtabwe alipokuwa akizikaguwa Bara bara za ndani zinazojengwa na msaada wa  Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo { IFAD } chini ya Usimamizi wa Wizara ya Kilimo na Mali Asili Zanzibar kupitia Mradi wa MIVARF akiwa katika ziara ya siku mbili kukaguwa shughuli za Maendeleo Kisiwani Pemba.

Alisema Serikali mbali ya kuendelea kuweka miundo mbinu ya Bara bara Kuu lakini pia  imeazimia kuzitengeneza bara bara za Vijijini pamoja na Mashambani kwa lengo la kuweka uwiano wa upataji wa huduma za usafiri kwa wananchi wa maene yote Nchini.
Balozi Seif alieleza kwamba huduma muhimu na za lazima kwa wananchi zitaendelea kusambazwa na Serikali ikiwa ni itekelezaji wa Ilani ya chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2010 iliyonadiwa na kupata ridhaa ya wananchi walio wengi Nchini.

Akigusia sekta ya uwekezaji Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  aliwaomba wananchi waendelee kushirikiana na wawekezaji  katika miradi wanayowekeza nchini ambayo husaidia kutoa ajira hasa kwa Vijana.

Alifahamisha kwamba Safari za Viongozi wakuu wa Kitaifa wakiwemo Mawaziri wa Wizara tofauti Nchini huzitumia katika kushawishi mashirika na makampuni kuja kuwekeza miradi hyao nchini kwa lengo la kuunga mkono uimarishaji wa Mapato ya Taifa.

Balozi Seif aliwatahadharisha wananchi wa Kisiwa kidogo cha Uvinje kiliopo Kaskazini ya Pemba kwamba hawana haki ya kukataa miradi iliyoamuliwa na Serikali kuwekezwa Kisiwani humo.

Alieleza kwamba hakuna Kikundi au Mtu anayeweza kuchukuwa hatua za kupinga maamuzi yanayotolewa na  Serikali katika matumizi ya ardhi ambayo ni mali ya Serikali kwa mujibu wa Sheria zilizopo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwataka wananchi hao washirikiane na mwekezaji aliyepewa fursa na Serikali kuwekeza Kisiwani humo na si busara kuisubiri Serikali Kuu itumie nguvu.

Mapema  Kaimu Afisa Mdhamini Wizara ya Kilimo na Mali Asili Pemba Nd. Mbarouk Ali Mgau alimueleza Balozi Seif kwamba Ujenzi wa Bara bara za ndani Kisiwani Pemba zenye urefu wa Kilomita 80 kwa kiwango cha kifusi utakaogharimu jumla ya shilingi Bilioni 6.4 unaendelea vyema.

Nd. Mbarouk alisema ujenzi huo Unaosimamiwa na Wizara ya Kilimo na Mali Asili Zanzibar umefadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo { IFAD }, Benki ya Maendeleo ya Afrika { ADB } kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Alisema zipo baadhi ya changamoto zinazosababisha vikwazo vya ujenzi wa Bara bara hizo akizitaja kuwa ni pamoja na umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi husika na wananchi katika kuzitunza bara bara hizo.

Naye Kaimu Mkurugenzi Mkaazi wa Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Pemba { ZIPA } Nd.Ali Shaaban Suleiman alisema Mkoa wa Kaskazini Pemba bado uko nyuma katika uwekezaji vitega uchumi.

Nd. Shaaban alisema uchelewaji wa uwekezaji miradi ya Kiuchumi ndani ya Mkoa huo hasa katika Sekta ya Utalii unaviza kutokana na baadhi ya wananchi wa mkoa huo kushutumu kwamba utalii umekuwa ukiharibu mila na silka za Wananchi hao.

Aliutaja Mradi wa uwekezaji ambao tayari umeshapata kibali kutoka Taasisi husika za Serikali ni ule wa Oxgen Holding Company wenye mtaji wa Dola za Kimarekani Milioni Tano utakaohusisha nyumba za kulala wageni pamoja na michezo mbali mbali ya Baharini.

Alisema mradi huo licha ya kupata vikwazo katika Kisiwa cha Uvinje lakini umelenga kutoa huduma za Maendeleo ya Wananachi pamoja na zile za kijamii na kuliongezea mapato Taifa.

Katika ziara hiyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipata fursa ya kuzitembelea bara bara za ndani kIsiwani Pemba za Mchangamdogo/Kinyikani hadi Mzambarauni, Bara bara ya Mkanjuni/ Kivumoni pamoja na ile ya Ole Kengeja inayogharamiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.