Na Mwandishi
Wetu, Tanga
MABINGWA
mara ya 24 wa ligi kuu soka Tanzania bara, Dar Young Africans wamevunja mwiko
wa Mgambo JKT kutofungwa na vigogo Simba, Yanga kwa misimu mitatu katika uwanja
wa CCM Mkwakwani Tanga baada ya kuifumua mabao 2-0 katika mechi ya ligi kuu
iliyomalizika jioni hii.
Mabao ya
Yanga yamefungwa kipindi cha pili na winga mwenye kasi Saimon Msuva na mtaalamu
wa magoli ya kichwa na mfungaji bora msimu uliopita, Amissi Tambwe.
Bao la
leo ni la 9 kwa Msuva na la 5 kwa Tambwe.
Msimu uliopita,
Yanga walipoteza dira ya kutwaa ubingwa kufuatia kuchapwa 2-1 na Mgambo katika
uwanja huu wa Mkwakwani, lakini leo wamelipa kisasi. Mgambo
waliwafunga Simba 2-0 jumatano ya wiki hii, lakini leo mambo yamewageukia kwa
kula kichapo kama hicho.
Kwa matokeo
waliyopata Yanga wameendelea kujikita kileleni kwa kufikisha pointi 37, pointi
nne mbele ya Azam fc watakaocheza na Coastal Union kwenye uwanja huo huo wa
Mkwakwani.
Hii
ilikuwa mechi 18 ya Yanga na Azam fc watacheza mechi ya 18 kesho. Kama watashinda
wataendelea kuwa nyuma kwa pointi moja na kama watatoa sare watakuwa pointi
tatu nyuma ya Yanga.
RIPOTI YA
MECHI
Mapema
dakika ya 3’ Mliberia Kpah Sherman alimgeuza beki wa Mgambo Novatus Lufunga
eneo la mita sita na kuachia shuti kali lililopaa juu ya lango.
Dakika ya
8’ Salim Aziz Gila alipiga shuti nzuri akiwa ndani ya eneo la hatari, lakini
bunduki yake haikulenga lango lililokuwa chini ya ulinzi wa Ally Mustapha
‘Bartez’.
Dakika 1’
baadaye Gila aliingia tena eneo la hatari akipomkea mpira mrefu kutoka katikati
ya uwanja, lakini shuti lake halikuwa na macho.
Dakika ya
11’ Mgambo walipata kona ya kwanza iliyochongwa na Malim Busungu, lakini kipa
Mustapha akaudhibiti mpira.
Baada ya
kona hiyo mpira ulibadilika na ukawa wa butuabutua kwa timu zote kutokana na
uwanja kuwa na maji na matope kulikosababishwa na mvua zinazoendelea ukanda wa
Pwani.
Mipira ya
chini ilikuwa inakataa, lakini Yanga walijitahidi kutuliza mpira chini na
haikuwa rahisi kupenya ngome ya Mgambo waliokuwa wanapiga bora liende kila mara
mpira ukifika katika eneo lao la hatari.
Dakika ya
30’ Kpah Sherman aliwachachafwa mabeki wa Mgambo Salim Kipanga na Ramadhan
Mlima, na beki akimpigia Saimon Msuva pasi eneo la 18’ lakini mfungaji huyo
bora wa Yanga akapiga shuti la juu kabisa.
Dakika 1’
baadaye Mgambo walifanya shambulizi la kushitukiza, lakini Gila alishindwa
kupiga vizuri kichwa.
Dakika Ya
36’ Mgambo walifanya shambulizi kali, Gila aliingiza krosi safi, lakini Nadir
Haroub ‘Cannavaro’ aliokoa na mpira ukawa kona ambayo haikuzaa matunda.
Dakika ya
38’ Bashiru Chanacha alimpanda mgongoni Sherman na mwamuzi Simon Mbelwa akaiona
na kuamua uwe mpira wa adhabu uliopigwa vizuri na Haruna Niyonzima, lakini
mlinda mlango Godson Mmasa aliudaka mpira huo kwa utulivu.
Dakika ya
39’ Said Juma Makapu alioneshwa kadi ya njano kwa kosa la kumchezea madhambi
beki wa kushoto wa Mgambo, Salim Mlima aliyekuwa anakwenda kujaza krosi kutoka
winga ya kushoto.
Almanusura
Yanga waandike bao dakika ya 42’, lakini Msuva alishindwa kutumia pasi nzuri ya
Sherman eneo la mita sita kutoka golini, mlinda mlango Mmasa akaudhibiti mpira.
Dakika ya
44’ Msuva alipata nafasi nyingine, lakini alipiga shuti mtoto ‘shuti mboga’ kwa
kipa Mmasa. Yanga wakarejea tena kushambulia, lakini mabeki wa Mgambo
walisimama imara.
Dakika 45’
za kipindi cha pili zilikamilika kwa suluhu (0-0).
Kiujumla
mpira haukuwa na ufundi kwa dakika zote za kipindi cha kwanza kutokana na
uwanja kuwa na matope.
Lakini
Yanga walitengeneza nafasi nyingi, lakini Msuva na Sherman walishindwa
kuzibadili kuwa magoli.
Mgambo
walifika langoni mwa Yanga na kutengeneza nafasi kadhaa, lakini kulikuwa na
ugumu wa kupiga mashuti kutokana na uimara wa mabeki Kelvin Yondan na
Cannavaro.
Nidhamu
ya ulinzi na kukaba vizuri kuliwaokoa Mgambo japokuwa walifanya makosa mengi ya
kumuachia nafasi Msuva ambaye unaweza kusema dakika 45’ za kipindi cha kwanza
hazikuwa upande wake.
Kipindi
cha pili mpira ulianza kiubabebabe kwa wachezaji wa timu zote na kila timu
ilitengeneza nafasi dakika za mapema, lakini umakini wa washambuliziaji ulikuwa
mdogo.
Dakika ya
45’ Amissi Tambwe alipiga shuti lililodhibitiwa na Kipa Mmasa. Dakika 1’
baadaye Fuluzuru Maganga alichuana na Cannavaro na beki huyo wa Yanga
akaonekana kumpiga na bega na Maganga akajiangusha kwa minajiri ya kupigwa,
lakini mwamuzi akamuonesha kadi ya njano akidai anamdanganya.
Dakika ya
50’ beki wa Mgambo Ramadhani Mlima alichezewa vibaya na Msuva na muamuzi Mbelwa
akamuonesha kadi ya njano winga huyo wa Yanga.
Dakika ya
56’ Mbuyu Twite alikwenda benchi na nafasi yake ikachukuliwa na Juma Jafar
Abdul. Mabadiliko
hayo yalitokana na Twite kuonekana hana ubora tangu kipindi cha kwanza.
Dakika ya
57’ Mgambo walifanya shambulizi zuri, lakini mabeki wa Yanga waliokoa shuti la
Ally Nassor aliyewafunga Simba goli safi siku ya jumatano.
Dakika ya
60’ bahati iliendelea kukosekana kwa Msuva, alimalizia vizuri krosi ya Juma
Abdul, mpira ukagonga mwamba wa juu pembeni upande wa kulia na kutoka nje.
Dakika ya
66’ Yanga walipanga mipango safi, Niyonzima akapiga krosi kutoka winga ya
kushoto, mabeki wa Mgambo wakatoa mpira nje na kuwa kona iliyozaa kizazaa,
lakini haikuzaa goli.
Dakika ya
68’ kocha wa Yanga, Hans van der Pluijm alimtoa nje Kelvin Yondan na nafasi
yake kuchukuliwa na Rajab Zahir. Mabadiliko haya yaliwashitua wengi, lakini
kiufundi tayari Yondan alikuwa ameanza kuhamanika, hivyo asingekuwa na msaada
zaidi kwa dakika zilizosalia.
Dakika ya
69’ Niyonzima alipiga shuti kali, kipa Mmasa alikwenda juu na kugusa mpira
ukatoka nje na kuwa kona ambayo haikuzaa matunda.
Yanga
walichangamka zaidi na kuendelea kulisakama lango la Mgambo, lakini walinzi wa
timu hiyo ya jeshi la kujenga Taifa walikomaa kama kawaida yao kuokoa hatari
zote.
Dakika ya
75’ Oscar Joshua alipiga krosi nzuri, Tambwe akapiga kichwa, lakini kipa Mmasa
akaudaka vizuri kabisa.
Dakika ya
77’ Saimon Msuva baada ya kosakosa za hapa na pale aliandika bao la kuongoza
kutokana.Uliingizwa
mpira wa kwanza mabeki wa Mgambo wakatoa, Juma Abdul akajaza tena mpira na
ukapigwa kichwa na Rajab Zahir na ndipo Msuva alipounganisha bila kutuliza na
gozi la ng’ombe kutinga nyavuni.
Dakika ya
79’ Sherman alitoka nje na nafasi yake ikachukuliwa na Hussein Javu.
Dakika ya
83’ Amissi Tambwe alipiga kichwa cha hatari na kujaza mpira nyavuni akiiandikia
Yanga goli la pili akiunganisha krosi ya Saimon Msuva.
Chanzo:Mpenja
blog.