Thursday 16 April 2015

UJENZI WA BARABARA YA DODOMA (MAYAMAYA) HADI BABATI (BONGA) KM 188.15 UNAENDELEA VIZURI

Mafundi wakiendelea na kazi za ujenzi wa daraja kubwa la Kolo lenye urefu wa mita 60 katika barabara ya Dodoma-Babati sehemu ya kipande cha barabara ya kutoka Mela kwenda Bonga chenye urefu wa km 88.8. 

Ujenzi wa daraja hilo unatarajiwa kukamilika mwezi Mei mwaka huu.Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Dodoma, Eng. Leonard Chimagu (watatu kutoka kushoto) akiwa na wahandisi wa barabara ya kutoka Mela-Bonga mara baada ya ukaguzi wa daraja la Kolo. Kazi ujenzi .


Ujenzi wa Barabara ya Dodoma (Mayamaya) hadi Babati km 188.15 katika sehemu ya Mayamaya-Mela  km 99.35  pamoja na kipande cha Mela Bonga km 88.8 unaendelea vizuri na unatarajiwa kukamilika mwaka 2017.

Kauli hiyo ilitolewa na Meneja wa Wakala wa Barabara Mkoani Dodoma Eng. Leonard Chimagu wakati akifanya ukaguzi wa ujenzi wa barabara hiyo inayojulikana kama barabara kuu ya Kaskazini  iliyoanzia Cape town nchini  Afrika Kusini hadi Cairo nchini Misri

“Katika barabara kuu hiyo sehemu yetu ya Tanzania ndio ilikua haina lami ila kwasasa ujenzi umeanza na unaendelea vizuri, ujenzi wa barabara katika sehemu ya kwanza ya Mayamaya-Mela km 99.35  umefikia asilimia 18 na ule wa Mela Bonga km 88.8 umefikia asilimia 20 ya ujenzi wake” alisema Eng. Chimagu.

Eng. Chimagu aliongeza kuwa  mkandarasi yupo katika hatua za mwanzo na anaendelea vizuri na  kama hakutakuwa na vikwazo vyovyote basi ataikamilisha barabara hiyo kwa wakati”, alisema Eng. Chimagu.

Kwa upande wa Mhandisi Mshauri katika sehemu ya barabara ya Mayamaya-Mela km 99.35   Eng. Godfrey Kombe alisema kuwa kazi za ujenzi zinaendelea vizuri na tayari mkandarasi ameshasafisha eneo la barabara lenye urefu wa km 70.

“Tayari Mkandarasi ameshasafisha eneo la barabara lenye urefu wa km 70 kwa kuondoa miti mikubwa, pia ameweza kujenga jumla ya makalavati 52 ya duara pamoja na 12 ya boksi”, alibainisha Eng. Kombe